Udongo

Udongo aina wa "Loess" kwenye mashamba ya Ujerumani ya kaskazini
Umbopande la udongo ni kanda zenye tabia mbalimbali zilizosababishwa na athari za mimea, wadudu na maji.

Udongo (pia: ardhi) ni sehemu ya juu kwenye uso wa nchi ambako mimea huweza kuota. Nao hutumiwa kwa kilimo.

Udongo wenyewe ni mchanganyiko wa vipande vidogo vya mwamba na madini yaliyosagwa pamoja na mata ogania kama mboji (mabaki ya mimea na wanyama yaliyooza) na pia wadudu na vijidudu vinavyoishi ndani yake. Udongo huwa pia na hewa na maji ndani yake zinazojaza nafasi kati ya vipande vidogo vya mwamba.

Kiasi chake kikubwa ni vipande vidogo vyenye asili ya mwamba au madini. Mwamba huvunjwa na maji, upepo na kutokana na athari ya joto / baridi kwa njia ya mmomonyoko. Hivi vipande vinaweza kuwa vidogo sana na kuonekana laini kama udongo wa ufinyanzi; au vigumu vyenye pembe kama punje za mchanga.

Udongo hupatikana kama tabaka juu ya mwamba unaofanya ganda la dunia. Mpaka wa chini wa udongo ni pale ambako mwamba mtupu unaanza; mpaka wa juu ni uso wa ardhi. Tabaka la udongo linaweza kuwa na unene wa kilomita kadhaa au sentimita chache tu.


© MMXXIII Rich X Search. We shall prevail. All rights reserved. Rich X Search