Kanisa la Asiria

Kanisa la Waashuru huko Moscow, Urusi.
Kanisa la Mashariki (kwa Dola la Roma) lilipofikia kilele cha uenezi wake.


Kanisa la Asiria, jina lake rasmi ni Kanisa Takatifu Katoliki la Mitume la Asiria la Mashariki[1],(kwa Kiaramu ܥܕܬܐ ܩܕܝܫܬܐ ܘܫܠܝܚܝܬܐ ܩܬܘܠܝܩܝ ܕܡܕܢܚܐ ܕܐܬܘܪܝܐ, ʻIttā Qaddishtā w-Shlikhāitā Qattoliqi d-Madnĕkhā d-Āturāyē), ni Kanisa la Waashuru ambalo kihistoria lilikuwa na kiini chake katika Mesopotamia ya kaskazini.

Kutoka huko wamisionari wake katika milenia ya 1 walieneza Ukristo hadi China, India na Indonesia.

Matukio mbalimbali yamepunguza idadi ya waamini wake hadi kufikia sasa 400,000 hivi (makadirio ni kati ya 200,000 na 500,000).

Ni kati ya Makanisa ya Kiorthodoksi ya Mashariki, lakini halina ushirika na Kanisa lingine lolote la kundi hilo wala la aina nyingine yoyote, ingawa kuna mapatano ya kiasi hasa na Kanisa Katoliki kupitia Kanisa la Wakaldayo ambalo linachanga nayo asili moja.

Linaongozwa na Patriarki wake, kwanzia mwaka 2015 Mar Gewardis III anayeishi Erbil, Iraq[2].

Chini yake kuna maaskofu wakuu, maaskofu, mapadri na mashemasi wanaotumikia majimbo na parokia katika nchi zote za Mashariki ya Kati na Kaukazi, India, Amerika Kaskazini, Oceania na Ulaya.

Upande wa teolojia, Kanisa hilo linafuata mafundisho yaliyotetewa na Patriarki Nestori wa Konstantinopoli hadi akatengwa na Kanisa Katoliki katika Mtaguso wa Efeso (431).[3]

Upande wa liturujia, linafuata ile ya Mesopotamia, ya Kisemiti kuliko zote.

  1. An Introduction to the Christian Orthodox Churches, By John Binns, page 28 [1]
  2. Baum, Wilhelm Baum (2003). The Church of the East: A Concise History. Routledge. ku. 150–155. ISBN 0-415-29770-2. Iliwekwa mnamo 22 Septemba 2010. {{cite book}}: Unknown parameter |coauthors= ignored (|author= suggested) (help)
  3. Cross, F. L. & Livingstone E.A. (eds), Oxford Dictionary of the Christian Church, Oxford University Press, 1997, p.351-352

© MMXXIII Rich X Search. We shall prevail. All rights reserved. Rich X Search