Roho Mtakatifu

Roho Mtakatifu akionekana kama njiwa, katika Basilika la Mt. Petro, Vatikano. Kazi ya Gian Lorenzo Bernini.

Roho Mtakatifu katika mapokeo ya dini ya Israeli, Ukristo na Uislamu ni roho ya Mungu pekee.

Kwa madhehebu karibu yote ya Kikristo, Roho Mtakatifu ni upendo wa Mungu, nafsi ya tatu ya Utatu Mtakatifu, mwenye Umungu mmoja na Baba na Mwana. “Pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi” (Rom 5:5). Ametumwa kwetu atufanyie kazi pasipo kuonekana. “Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho” (Yoh 3:8). “Wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu” (Rom 8:14).

Hata hivyo, tofauti katika teolojia ya madhehebu hayo kuhusu Roho Mtakatifu ni kubwa kuliko zile zilizopo kuhusu Nafsi mbili za kwanza (Mungu Baba na Mungu Mwana)[1].

Kwa jumla Roho Mtakatifu anasadikiwa kuvuviwa milele na Baba kwa njia ya Mwana awe mwalimu wa wanadamu kwa kuwafundisha, kuwakumbusha na kuwazuia kufanya mambo mabaya au dhambi.

Kazi zote za Roho Mtakatifu zinahusiana na Yesu na kulenga hasa kuandaa watu wampokee, wamfuate na kumshuhudia katika umoja wa kundi lake, Kanisa. “Ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia” (Yoh 15:26-27).

  1. Pontifical Council for Promoting Christian Unity: The Greek and the Latin Traditions regarding the Procession of the Holy Spirit Archived 3 Septemba 2004 at the Wayback Machine. and same document on another site

© MMXXIII Rich X Search. We shall prevail. All rights reserved. Rich X Search