Tafsiri

Jiwe la Rosetta kutoka Misri ya Kale ni kati ya mifano ya kwanza ya tafsiri (ina matini ileile kwa lugha tatu).

Tafsiri (Asili ya neno hili ni Kiarabu; kisawe cha neno hili ni Tarjuma) ni kazi ya kutoa maana ya maneno kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine.

Mtu anayefanya kazi hii huitwa mfasiri au mkalimani.

Kutafsiri kuna maana mbili kwa mujibu wa Kamusi Kuu ya Kiswahili (KKK):

  1. Ni kutoa andiko au maelezo fulani katika lugha nyingine kwa maana ilele.
  2. Toa maelezo ya lugha fulani kwa lugha nyingine kwa maana ileile kwa kutumia maandishi. Katika maana ya pili, maana yake ni kitenzi elekezi, ni kitenzi ambacho kinapokea Yambwa, yaani nomino ya mtendwa.

Katika misingi ya kielimu dhana ya tafsiri imeweza kujadiliwa na wataalamu mbalimbali.

  • Newmark (1982): Tafsiri ni jaribio la kuwasilisha ujumbe uleule ulioandikwa katika lugha moja kwa lugha nyingine.
  • Mwansoko na wenzake (2006): Tafsiri ni zoezi la uhawilishaji (Transferring) wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja hadi lugha nyingine.
  • Uhawilishaji ni kuhamisha mawazo au ujumbe kutoka katika lugha moja kwenda lugha nyingine.
  • Mfasiri ni mtu mwenye ujuzi mzuri wa lugha zaidi ya moja anayefanyakazi ya kutafsiri matini kutoka lugha moja kwenda nyingine. Mara nyingi mtu anayefanya kazi ya kutafsiri huwa anahawilisha matini kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine. Hasa katika maandishi.
  • Matini ni maandishi yaliyomo katika andiko linalohusu jambo fulani. Matini inaweza kuwa riwaya, tamthiliya au ushairi. Kimsingi chochote kilichoandikwa ili kiweze kutolewa tafsiri huitwa matini.

© MMXXIII Rich X Search. We shall prevail. All rights reserved. Rich X Search